MRADI WA TRILIONI 1.15 WA UBORESHAJI WA ELIMU NCHINI WAZINDULIWA.

Mkurugenzi Mkaazi wa Benki ya Dunia, Mara Warwick.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda

 


Na Zulfa Mfinanga

Arusha.

Serikali imezindua mradi wa kuboresha upatikanaji wa fursa sawa katika utunzaji bora wa elimu ya awali na msingi Tanzania Bara (BOOST) utaogharimu takribani sh.trilioni 1.15 utakaotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano.



Akizindua mradi huo leo Jijini Arusha, Waziri wa elimu , Sayansi na Teknolojia,Prof.Adolf Mkenda amesema mradi huo umefadhiliwa na benki ya dunia kwa lengo kuimarisha nyanja mbalimbali katika sekta ya elimu kuanzia ngazi ya elimu ya awali.


Prof. Mkenda amesema mradi huu utasaidia kuongezeka kwa uwiano wa uandikishwaji wa wanafunzi wa elimu ya awali kutoka asilimia 76.9 hadi 85 pamoja na kuongeza kiwango cha wanafunzi kubaki shuleni katika halmashauri zilizo katika kundi la robo ya chini kutoka asilimia 55.9 hadi 66.2.


Kamishna wa elimu Tanzania Dk.Lyabwene Mtahabwa  amesema mradi wa BOOST ni mpango wa lipa kulingana na matokeo katika elimu yaani (EPforR II) ikiwa maandalizi ya utekelezaji yameshakamilika kutokana na majadiliano mbalimbali kati ya serikali na Benki ya dunia katika uendeshaji wake.


"Baadhi ya changamoto zilizopelekea kuwepo kwa Mradi huu ni pamoja na kuwepo kwa msongamano wa wanafunzi madarasani kutokana na uhaba wa miundombinu ya madarasa, baadhi ya shule kutokuwa na mazingira rafiki ya ujifunzaji na ukosefu wa vifaa vya ufundishaji wa elimu ya awali" amesema Dkt Mtahabwa


Mkuu wa Wilaya ya Arusha Said Mtanda aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongella ameishukuru Wizara ya Elimu, TAMISEMI pamoja na Benki ya Dunia kwa kuleta mradi huo na kusema wapo tayari kuusimamia katika kuleta chachu ya maendeleo kwenye sekta ya elimu.


Naye Mkurugenzi Mkaazi wa Benki ya Dunia, Mara Warwick amesema mradi huu utaongeza nafasi ya watoto wengi kupata elimu ya awali na msingi pamoja na kuongeza ushindani wa uwajibikaji kwa walimu.


Mradi huu utawanufaisha zaidi ya wanafunzi milioni 12 kote nchini na itasaidia kuongezeka kwa uwiano wa uandikishwaji wa wanafunzi wa elimu ya awali kutoka asimilia 76.9 hadi asimilia 85.


Matokeo mengine ya mradi huu ni kuongeza kiwango Cha wanafunzi kubaki shuleni katika halmashauri zilizo katika kundi la robo ya chini kutoka asilimia 55.9 hadi asilimia 66.2 pamoja na kuanzishwa kwa vituo vya walimu kwa ajili ya utoaji wa mafunzo kwa njia ya TEHAMA kupitia maktaba mtandao.

This is received, thanks for your comments, will come back to you

Previous Post Next Post